Maktaba ya chuo cha ualimu Korogwe yazinduliwa

0
265

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa Majaliwa, amezindua maktaba mpya ya chuo cha Ualimu Korogwe kilichopo mkoani Tanga.

Akizungumza na baadhi ya walimu tarajali pamoja na wanafunzi aliowakuta katika maktaba hiyo mara baada ya kuizindua, Waziri Mkuu amewataka kutumia vizuri maktaba hiyo.

Naye Katibu Mkuu wa wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt Leonard Akwilapo amesema kuwa,
serikali imetoa zaidi ya shilingi milioni mia tatu kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa maktaba hiyo ambayo ujenzi wake ulianza kwa michango ya wananchi wa Korogwe.

Dkt Akwilapo ameongeza kuwa, serikali iliamua kutoa kiasi hicho cha fedha ili kuunga mkono juhudi za wananchi ambao walichanga shilingi milioni 1.9 kwa ajili ya kuanza ujenzi huo.

Maktaba hiyo ya chuo cha Ualimu Korogwe ina vifaa vya kisasa zikiwemo kompyuta zinazowezesha matumizi maktaba mtandao.

Maktaba hiyo itatumiwa na walimu tarajali zaidi ya elfu moja ambao wanasoma masomo ya sayansi, hisabati na Teknolojia ya habari na Mawasiliano pamoja na wanafunzi wa shule za msingi na sekondari wilayani Korogwe.