Majaliwa aagiza mkandarasi kurejea eneo la kazi

0
204

Waziri Mkuu Kassimu Majaliwa ameagiza mkandarasi M.A Kharafi and Sons aliyekuwa akitekeleza mradi mkubwa wa maji wa Mwanga-Same-Korogwe ambao utahudumia wananchi zaidi ya laki nne kuendelea na kazi.
 
Waziri Mkuu Majaliwa ameyasema hayo wilayani Mwanga wakati akikamilisha ziara yake mkoani Kilimanjaro ambapo amekagua mradi huo na kusema kuwa lengo ni kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji safi na salama kwa wakati.
 
Amemuagiza waziri wa maji kukaa pamoja na mkandarasi huyo  na kuzungumza hatua iliyobaki ili kuhakikisha kazi inaanza haraka iwezekanavyo.
 
Akizungumzia kukosekana kwa umeme katika chanzo cha maji cha mradi huo, Waziri Mkuu ameiagiza wizara ya nishati kuweka mfumo wa umeme kwenye mashine haraka iwezekanavyo ili uweze kusukuma maji katika mradi huo.
 
Awali akizungumzia mradi huo Waziri wa Maji, Jumaa Aweso amesema kwa sasa mradi huo umetekelezwa kwa asilimi 64 na amewahakikishia wakazi wanaozunguka chanzo cha mradi huo kuwa wa kwanza kupata maji.