Magoti, sarakasi marufuku bungeni

0
179

Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Tulia Ackson amepiga marufuku wabunge wa bunge hilo kufanya vituko wakiwa ndani ya ukumbi wa bunge kama kupiga magoti au sarakasi wakati wakichangia mijadala mbalimbali.

Dkt. Tulia ametoa maelekezo hayo baada ya mbunge wa jimbo la Igalula, Venant Protas kuomba mwongozo wa Spika akitaka kujua kama bunge linaruhusu wabunge kuchangia mijadala kwa kufanya vituko wakiwa ndani ya ukumbi wa bunge.

Mbunge Protas aliomba muongozo huo kufuatia mbunge wa jimbo la Mbulu Vijijini, Flatei Massay kupanda juu ya meza na kupiga sarakasi wakati akichangia mjadala wa bajeti wa wizara ya Ujenzi na Uchukuzi kwa mwaka wa fedha wa 2022/2023.

Tukio jingine ni la mbunge wa viti maalum Jacqueline Msongozi ambaye alipiga magoti wakati akiwasilisha hoja yake.