Maafisa masijala kula viapo

0
234

Rais Samia Suluhu Hassan amewataka maafisa masijala kufanya kazi kwa weledi kwani wao ni kitovu cha utumishi.

Rais Samia ameyasema hayo jijini Arusha wakati akifungua rasmi mkutano.mkuu wa 10 wa chama cha Taaluma ya Menejimenti ya Kumbukumbu ya Nyaraka Tanzania (TRAMPA).

Akijibu moja ya hoja iliyotolewa na
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Katiba, Sheria, Utumishi na Utawala Bora wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Haroun Ali Suleiman kuhusu watumishi wa masijala kula kiapo, Rais Samia amesema jambo hilo litafanyika wakati wa mkutano ujao utakaofanyika mwaka 2023.

“TRAMPA na TAPSEA tuwachanganye wote pamoja wafanye mkutano mkubwa pale Zanzibar, kwa maana hiyo huo ndio utakuwa mkutano wetu wa kula kiapo. Mtakula kiapo pale.” amesema Rais Samia

Amewasihi wanataaluma hao kuwa waadilifu katika utunzaji wa kumbukumbu.

“Niwaombe na niwaase watunza kumbukumbu wenzangu sisi mama zenu hatukufanya hivyo. Tunzeni siri za serikali.” amesisitiza Rais Samia Suluhu Hassan

Kwa upande wake Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Jenista Mhagama ameeleza kuwa, kwa sasa maafisa masijala wenye stashahada na shahada watatengwa madaraja.