Kamati ya bunge kumhoji CAG

0
1012

Spika wa bunge Job Ndugai amemtaka Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Profesa Mussa Assad kufika katika Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge tarehe 21 Januari ili kutoa ufafanuzi kuhusu kauli yake anayodaiwa kuitoa katika mahojiano na chombo kimoja cha habari nchini Marekani.

Spika Ndugai ametoa kauli hiyo jijini Dodoma wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu kauli ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali inayodaiwa kulidhalilisha bunge.

Pia ametoa ushauri kwa wananchi na taasisi mbalimbali za serikali kuwa ni ustaarabu na kutoisema vibaya nchi, nje ya nchi.

Halikadhalika Spika Ndugai amemtaka mbunge wa Kawe Halima Mdee kufika katika Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya bunge tarehe 22 Januari ili kuthibitisha maneno anayodaiwa kusema katika mitandao ya kijamii kuhusu bunge.