Kagaigai: Kashirikianeni na wenzenu

0
290

Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro, Stephen Kagaigai amewataka wakuu wa wilaya kusikiliza na kutatua kero mbalimbali za Wananchi katika maeneo yao ya kiutawala, ili kuwaletea Wananchi maendeleo.

Kagaigai ameyasema hayo mjini Moshi mkoani Kilimanjaro wakati akiwaapisha wakuu wa wilaya walioteuliwa hivi karibuni na Rais Samia Suluhu Hassan kushika nyadhifa hizo.

Mkuu wa wilaya ya Mwanga mkoani Kilimanjaro, Abdallah Mwaipaya akila kiapo baada ya kuteuliwa hivi karibuni na Rais Samia Suluhu Hassan kushika wadhifa huo.

Kagaigai amesema ni vema wakuu wa wilaya hao wahakikishe wanazielewa kero za Wananchi na kuzitatua kwa weledi, uadilifu bila ubaguzi wala upendeleo wowote.

Amesema ili yote hayo yakamilike wakuu hao wa wilaya wanapaswa kushirikiana na Makatibu Tawala, Wakurugenzi Watendaji wa halmashauri na wakuu wa taasisi zilizoko katika wilaya zao kwa kutumia madawati ya kero.

Mkuu wa wilaya ya Rombo mkoani Kilimanjaro Kanali Hamis Maiga akila kiapo baada ya kuteuliwa hivi karibuni na Rais Samia Suluhu Hassan kushika wadhifa huo.

Wakuu wa wilaya wawili kati ya sita mkoani Kilimanjaro ndio wamekula kiapo, huku wengine wanne wakiwa wamehamishiwa katika wilaya za mkoa huo kutoka vituo vingine.