IGP Sirro aagiza mikutano kujadili usalama

0
226

Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini Simon Sirro amewaagiza wakuu wa polisi wa wilaya mkoani Kilimanjaro kufanya vikao kila mwezi na viongozi wa ngazi za kata, ili kujadili masuala mbalimbali ya ulinzi na usalama katika maeneo yao.

Kamanda Sirro ameyasema hayo mjini Moshi wakati alipokutana na viongozi wa dini, mitaa, vijiji, kata na tarafa mkoani Kilimanjaro.

Kamanda Sirro amesema mkuu wa polisi wa wilaya yoyote ambaye hatakutana na viongozi hao, hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yake.

“Lazima tuheshimiane Mwenyekiti wa Serikali ya mtaa, mtendaji wa kata ni watu muhimu katika kulinda na kusimamia usalama wa raia, hivyo Jeshi la Polisi ni lazima liwasikilize viongozi hao.” Amesema IGP Sirro.

Amesema iwapo viongozi hao wakiamua kurudi nyuma katika mapambano dhidi ya uhalifu, polisi pekee hawataweza kutatua changamoto za uhalifu nchini.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya amani wilayani Moshi, Askofu Jones Mola amesisitiza Wananchi wa mkoa huo kuwekeza katika kudumisha ulinzi na usalama kama mtaji katika kuleta maendeleo ya Taifa.