Haki za wanyama wanaofugwa

0
119

Wanyama wa nyumbani wapo wa makundi kadhaa wakiwemo wale rafiki kama mbwa, wanyama wanaofanya kazi kama punda na wanyama wanaozalisha kama vile ng’ombe na mbuzi.

Akizungumza kwenye mahojiano na TBC 1 katika kipindi cha Jambo Tanzania, Daktari wa mifugo Geofrey Josiah amesema, wanyama wote hao wanaofugwa wana haki na kanuni za msingi za kuishi nao.

Haki hizo ni pamoja na ile ya kupata chakula na maji. Amesema mnyama lazima apate chakula ili kutengeneza lishe itakayompa kinga na afya bora.

Dkt. Geofrey amesema mnyama hatakiwi kuishi kwa kubughudhiwa ikiwa ni pamoja na kuwapiga. Ameeleza kuwa si lazima kumpiga mbwa kwani unaweza kumfunza kwa kutumia mbinu nyingine.

Haki ya kutibiwa. Hii ni kwa ajili ya afya ya mnyama lakini pia kumkinga binadamu na maambukizi ya magonjwa yanayotoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu kama vile kichaa cha mbwa.

Daktari huyo wa mifugo pia ameshauri kuwekwa rekodi za mnyama ikiwa ni pamoja na tarehe ya kuzaliwa, kama ni wanyama wa maziwa je anatoa maziwa kiasi gani na uzao wake ukoje.