Gamba kuzikwa Jumatano Bunda

0
1799

Mwili wa Mtangazaji wa Tanzania aliyekuwa akifanya kazi katika Idhaa ya Kiswahili ya Sauti ya Ujerumani (DW) , – Isaac Gamba unaagwa hii leo jijini Dar es salaam.

Mwili wa Gamba unaagwa baada ya kuwasili nchini usiku wa kuamkia hii leo ukitokea nchini Ujerumani.

Mara baada ya ibada pamoja na kukamilika kwa shughuli ya kuaga  katika eneo la Lugalo, mwili wa Gamba utasafirishwa kwenda mkoani Mara kwa ajili ya mazishi yatakayofanyika Jumatano Oktoba 31.

Gamba aliyekuwa mtangazaji wa michezo na burudani katika Idhaa hiyo ya Kiswahili ya Sauti ya Ujerumani  alikutwa akiwa amefariki dunia mjini Bonn nchini Ujerumani Oktoba 18 mwaka huu baada ya kutoonekana ofisini kwa muda wa siku mbili.

Hali ya kutoonekana ofisini iliwashtua wafanyakazi wenzake ambao waliamua kutoa taarifa polisi ambao walifika nyumbani kwake na kuvunja mlango na ndipo walimkuta amekwishafariki dunia.

Gamba aliyezaliwa mwaka 1970 wilayani Bunda, ni mtoto wa 12 kati ya watoto 13 na alijiunga na Idhaa ya Kiswahili ya Sauti ya Ujerumani mwaka 2015 akitokea kwenye kituo cha ITV na Radio One nchini Tanzania.