Fedha za pole kuanza kutolewa

0
2281

Malipo ya fedha za pole kwa kila familia iliyopoteza ndugu au jamaa kufuatia ajali ya kuzama kwa kivuko cha MV Nyerere Septemba 20 mwaka huu yanaanza kufanyika hii leo.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe amesema kuwa malipo ya fedha hizo yanafanyika chini ya usimamizi wa mkuu wa mkoa wa Mwanza,- John Mongela.

Rais John Magufuli ametangaza malipo ya shilingi milioni moja ambazo zitatolewa kwa kila familia kwa ajili ya kila marehemu, fedha ambazo ni tofauti na zile zilizotangazwa kutolewa awali ambazo zilikua ni shilingi laki tano.

Rais Magufuli pia ametangaza malipo ya shilingi milioni moja kwa kila aliyenusurika katika ajali hiyo ya kuzama kwa kivuko cha MV Nyerere huko Ukerewe mkoani Mwanza.

Habari zaidi kutoka wilayani Ukerewe zinasema kuwa jitihada za kukinasua kivuko hicho zinaendelea ambapo Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Jenerali Venance Mabeyo amesema kuwa hatua iliyofikiwa ni ya kuridhisha.