Dodoma yazizima, maelfu wamuaga JPM

0
279

Maelfu ya wakazi wa jiji la Dodoma wamejitokeza kwa wingi kuuaga mwili wa aliyekuwa Rais wa Tanzania Dkt John Magufuli katika shughuli ya kitaifa iliyofanyika kwenye uwanja wa Jamhuri.

Mapema asubuhi ya leo, wakazi wa mkoa huo wa Dodoma na maeneo jirani walijitokeza katika mitaa na barabara mbalimbali maarufu za mkoani humo kuuga mwili wa Mpendwa wao Dkt Magufuli.

Mwili wa Dkt Magufuli umeagwa kwa heshima na viongozi kutoka ndani na nje ya nchi, ambapo kila aliyepata nafasi amemuelezea kuwa alikuwa ni mtu aliyewapenda watu wake na alikuwa mwana Afrika wa kweli.

Baada ya viongozi hao kutoka ndani na nje ya nchi kuaga mwili wa Dkt Magufuli, mwili huo umezungushwa mara tano kwenye uwanja wa Jamhuri na kisha kuzungushwa katika viunga vya jiji la Dodoma ili kutoa fursa kwa Wananchi kutoa heshima zao za mwisho.

Hapo kesho mwili wa Dkt Magufuli utaagwa na Wakazi wa Zanzibar katika uwanja wa Amaan.