Chanjo ya Polio kutolewa kwenye mikoa sita

0
145

Wizara ya Afya kwa kushirikiana Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) inatarajia kuendesha kampeni ya kutoa chanjo dhidi ya ugonjwa wa Polio kwa watoto zaidi ya Milioni tatu nchini, walio na umri wa chini ya miaka 8.

Watoto watakaopatiwa chanjo hiyo ni wa mikoa ya Rukwa, Kagera, Kigoma, Katavi, Songwe na Mbeya.
 
Waziri wa Afya Ummy Mwalimu amesema kampeni hiyo itaanza Septemba 21 hadi 24, 2023.
 
Tanzania inaendesha kampeni hiyo ya chanjo kutokana na wizara ya Afya kupokea taarifa Mei 26, 2023 za uwepo wa mtoto mmoja mwenye umri wa mwaka mmoja na miezi kumi na moja ambaye alionesha dalili za kupooza kwa ghafla katika manispaa ya Sumbawanga, mkoani Rukwa.

Uchunguzi wa Maabara ulithibitisha kuwa mtoto huyo ana maambukizi ya virusi cha Polio. 

Waziri Ummy amesema maambukizi ya virusi vinavyosababisha ugonjwa wa Polio yametolewa taarifa pia katika nchi zinazopakana na Tanzania.