Burundi yapata Waziri Mkuu mpya

0
132

Bunge la Burundi, limemuidhinisha Waziri Mkuu mpya wa nchi hiyo ambaye ni Gervais Ndirakobuca, aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani wa nchi hiyo.

Ndirakobuca anachukua nafasi ya Alain Guillaume Bunyoni ambaye mapema hii leo alifukuzwa kazi na Rais Évariste Ndayishimiye wa Burundi.

Rais Ndayishimiye amemfukuza kazi
Bunyoni zikiwa zimepita siku chache baada ya kuwatuhumu viongozi kadhaa wa ngazi ya juu nchini humo kwa kupanga njama za kumpindua.

Katika kura zilizopigwa na wabunge wa bunge la Burundi mapema hii leo ili kuunga mkono uamuzi wa Rais Ndayishimiye,
wabunge wote 113 kutoka chama tawala wameunga mkono uamuzi huo.

Hata hivyo hazijatolewa sababu zozote za Waziri Mkuu huyo wa Burundi kufukuzwa kazi.

Wiki iliyopita, Rais Ndayishimiye alikaririwa akisema kuwa atahakikisha anawashughulikia watu wote wanaopanga njama za kumuondoa madarakani.