Bilioni 1.35 yatengwa kukuza michezo kimataifa

Michezo

0
186

Serikali imeongeza uwekezaji kifedha katika michezo kwa zaidi ya 500% kwa kipindi cha fedha cha mwaka 2021/22.

Akizungumza mbele ya Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, Ikulu jijini Dar es salaam, Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo, Innocent Bashungwa amesema tayari Serikali imeelekeza kiasi cha bilioni 1.35 kuzihudumia timu za Taifa za michezo mbalimbali.

Awali, katika mwaka wa fedha 2020/2021 serikali ilielekeza milioni 277 kukuza timu za Taifa.

Aidha, Rais Samia Suluhu Hassan amesema tayari kuna mipango mikubwa ya kukuza sekta ya michezo ikiwa ni pamoja na kujenga viwanja vitatu vikubwa vya michezo nchini vitakavyoweza kutumika kwenye mashindano ya kimataifa pamoja na kujenga ‘Sports Arena’ Dar es Salaam na Dodoma.

Kwa upande mwingine Rais Samia amewataka viongozi wa vilabu vya michezo kuwaangalia wachezaji wakike haswa wa soka waweze kunufaika na mfuko wa michezo.

Rais Samia ameahidi kudhamini mashindano ya CECAFA kwa upande wa wanawake pindi yatakapoanza.