Bashungwa: Zinazofunguliwa ni ‘Online TV’ tu

0
193

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Innocent Bashungwa amesisitiza kuwa agizo la Rais Samia Suluhu Hassan la kutaka kufunguliwa kwa vyombo vya habari vilivyofungiwa tayari limefanyiwa kazi.

Waziri Bashungwa ametoa kauli hiyo mkoani Dar es salaam wakati wa mkutano wake na Waandishi wa habari, ikiwa ni siku moja tu baada ya agizo hilo la Rais Samia Suluhu Hassan.

Amefafanua kuwa vyombo vya habari vitakavyofunguliwa ni Televisheni za mtandaoni (online TV) pekee na si vinginevyo.

Kwa upande wa magazeti yaliyofungiwa, Waziri Bashungwa amesema Watendaji wa magazeti hayo wanatakiwa  kufika  Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ili kuangalia sababu zilizosababisha kufungiwa kwa vyombo hivyo na kuweza kuangalia nini kifanyike kuhusu jambo hilo.

Waziri Bashungwa ameongeza kuwa lengo la Rais Samia Suluhu Hassan pamoja na wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ni kuboresha tasnia ya habari, huku taaluma hiyo ikisimamiwa kwa kufuata sheria.

Aidha, ameongeza kuwa wizara yake itashirikiana na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kuangalia sheria zinazopaswa kufuatwa na Televisheni za mtandaoni pamoja na gharama za usajili ili kuendelea kuboresha vyombo hivyo vya habari.