Bara, Zanzibar kukabili kwa pamoja mabadiliko ya tabianchi

0
141

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Selemani Jafo amesema kwa sasa suala la mazingira linashughulikiwa kwa pamoja na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ili kulifanya suala hilo kuwa na sura ya kitaifa.

Akijibu swali la Mbunge wa jimbo la Nungwi Simai Hassan Sadiki aliyetaka kujua serikali inashirikiana vipi na Zanzibar katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi ikiwa suala la mazingira sio la Muungano, Jafo amesema pamoja na kwamba suala hilo sio la muungano lakini ushirikiano upo na miradi kadhaa inafanywa kwa pamoja.

Jafo amesema, kwa sasa Serikali ya Muungano kwa kushirikiana na ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar wanatekeleza miradi kadhaa ya kimazingira kisiwani Pemba lakini pia vikao vyote vya kisekta wanakutana na watendaji wa Zanzibar ili kufanya maamuzi kwa pamoja.