Balozi Job Lusinde afariki dunia

0
585

Nguli wa siasa nchini Tanzania, Balozi Mstaafu, Job Lusinde amefariki dunia leo Julai 7, 2020 akiwa na umri wa miaka 90.

Balozi Lusinde ambaye aliunda baraza la kwanza la mawaziri la Mwalimu Julius Nyerere mara baada ya uhuru akiwa Waziri wa Serikali za Mitaa amefariki katika Hospitali ya Mloganzila jijini Dar es Salaam alipokuwa akipatiwa matibabu.

Taratibu za mazishi zinafanyika katika makazi yake Kilimani jijini Dodoma.

Balozi huyo ambaye alikuwa mtoto wa mchungaji alizaliwa Oktoba 9, 1930 katika Mtaa wa Kikuyu, Dodoma.

Miongoni mwa nyadhifa ambazo amewahi kuzishika ni pamoja na kuwa Balozi wa Tanzania nchini China kuanzia 1975 hadi 1984, Waziri wa Mawasiliano na Kazi na Waziri wa Mambo ya Ndani.