Ajali yaua 14 Busega

0
205

Watu 14 wamefariki dunia katika ajali ya gari iliyotokea kwenye kijiji cha Shimanyire wilaya ya Busega mkoani Simiyu.

Mkuu wa wilaya Busega, Gabriel Zakaria ameiambia TBC kwa njia ya simu kuwa ajali hiyo imehusisha gari lililokuwa katika msafara wa mkuu wa mkoa wa Mwanza, Mhandisi Robert Gabriel ambaye alikuwa akielekea wilayani Ukerewe kukabidhi miradi mbalimbali ya maendeleo.

Amesema gari hilo lililokuwa limebeba Waandishi wa habari, limegongana uso kwa uso na gari ndogo ya abiria aina ya Hiace lililokuwa likifanya safari zake kati ya eneo la Nyamikoma na Magu, ambapo waandishi wa habari watano wamefariki dunia papo hapo.

Mkuu huyo wa wilaya ya Busega ameongeza kuwa, majeruhi wa ajali hiyo wanapatiwa matibabu katika hospitali ya rufaa ya Bugando iliyopo mkoani Mwanza na wengine kwenye kituo cha afya cha Nassa wilayani Busega.

Amesema kwa sasa jeshi la polisi lifanya uchunguzi ili kubaini chanzo cha ajali hiyo.