Watu wawili wafariki kwa Corona Afrika Kusini

0
724

Waziri wa afya nchini Afrika Kusini ametangaza vifo vya kwanza vya COVID-19 nchini humo asubuhi ya leo.

Taarifa ya Waziri Zwelini Mkhize kwa vyombo vya habari imeeleza kuwa mwanamke mmoja amefariki akiwa kwenye hospitali ya umma na mwingine katika hospitali binafsi.

Vifo hivyo vinasemekana kuwa vya wanawake wawili wenye umri wa miaka 28 na 46, kutoka mkoa wa Western Cape.

Afrika Kusini hadi kufikia leo inaongoza kwa kuwa na visa vingi zaidi Afrika. Katika taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari, Mkhize amesema visa vya COVID-19 vimeongezeka nchini humo kutoka 927 jana Machi 26 na kufikia zaidi ya 1000 leo asubuhi.

Wakati nchi hiyo ikiwa na visa takribani 1000, nchi nyingine za Afrika kama vile Burundi, Comoro, Malawi, Lesotho, Botswana, Sudan Kusini na Siera Leone bado hazijaripoti kuwa na wagonjwa wa Corona.

Picha na Bloomberg