Wanasayansi wakutana Cape Town

0
383

Rais Cyril Ramaphosa wa Afrika Kusini amesema kuna umuhimu kwa wanasayansi wa bara la Afrika na nje ya Afrika kuhakikisha vumbuzi zinazovumbuliwa barani humo zinatambulika na kukubalika duniani kote, ili kuwe na usawa wa masuala ya sayansi duniani.

Rais Ramaphosa ameyasema hayo alipokuwa akifungua mkutano wa kimataifa wa sayansi kwa mwaka 2022 mjini Cape Town, Afrika Kusini ambapo ni mara ya kwanza kufanyika barani Afrika.

Akihutubia wadau wa masuala ya sayansi kutoka nchi zaidi mia moja duniani, Rais Ramaphosa amebainisha kuwa kumekuwepo na vumbuzi mbalimbali ambazo zimekuwa zikifanywa na waafrika, lakini hazitambuliki licha ya kuwa na umuhimu katika kutatua changamoto za kijamii, hivyo ni vema wanasayansi wote wakatambuliwa kwa usawa.

Aidha Rais Ramaphosa amesema, ili vumbuzi za kisayansi zitatue changamoto za kijamii ikiwemo mabadiliko ya tabianchi, ni muhimu kukawa na ushirikiano wa pamoja.

Mkutano wa Kimataifa wa Sayansi kwa mwaka 2022, umebeba kauli mbiu inayosema Sayansi kwa Haki ya Kijamii.