Tsunami yasababisha hofu Indonesia

0
1201

Hali ya wasiwasi imeongezeka nchini Indonesia baada ya nchi hiyo kukumbwa na tetemeko la chini ya bahari Tsunami, kwa kuwa kuna uwezekano wa kutokea Tsunami nyingine.

Wanasayansi nchini Indonesia wamesema mlima Anak Krakatau wenye volkano hai ulioko chini ya bahari umelipuka na kusababisha Tsunami hiyo iliyotokea usiku wa kuamkia jana na kusababisha vifo vya watu 373.

Wanasayansi wamesema volkano ya mlima Anak Krakatau, jina linalomaanisha mtoto wa Krakatau inaonyesha dalili ya kuanza kulipuka tena na haifahamiki, safari hii italeta athari gani, kwani mlipuko wa kwanza ulitokea bila taarifa.

Habari zinasema katika pwani ya nchi hiyo matope ya moto kutoka baharini yanaweza kuonekana yakirushwa juu na hivyo watu hawajui watajisalimisha vipi.

Maelfu ya watu bado wako katika makazi ya muda baada ya maelfu ya nyumba kusombwa na maji yaliyokumbwa na Tsunami hiyo kutoka baharini na kwenda katika nyumba za watu na kusomba na hoteli pia.

Zoezi la kuwatambua watu waliokufa kwa Tsunami linaendelea na waokoaji wanaendelea kwa kazi ya kuwatafuta watu walionusurika na tukio hilo, kabla haujatokea mlipuko mwingine.