Trump asisitiza kutovunja sheria

0
2713
U.S. President Donald Trump listens during a cabinet meeting at the White House in Washington, U.S., July 18, 2018. REUTERS/Leah Millis - RC1459858650

Rais Donald Trump wa Marekani amesisitiza kuwa malipo yanayodaiwa kufanywa kwa siri kwa wanawake wawili wanaodhaniwa kuwa na uhusiano naye hayakuvunja sheria ya fedha za kampeni za uchaguzi mwaka 2016.

Trump amekana tuhuma za kuhusika kwake katika kutumia fedha zilizotengwa kwa ajili ya mikutano ya kampeni kuwalipa wanawake hao.

Mapema wiki hii katika kesi iliyosikilizwa kwenye mahakama moja mjini New York , mwanasheria wa zamani wa Rais Trump,- Michael Cohen alidai kuwa Trump alimpa maelekezo ya kutoa fedha kwa lengo la kuwashawishi wanawake hao kukaa kimya wakati wa uchaguzi huo wa Urais wa mwaka 2016.

Ikulu ya Marekani imesisitiza kuwa kuvunja sheria ya fedha za kampeni kwa Cohen hakumaanishi kuwa Rais Trump naye atawajibika,

Hata hivyo Rais Trump mwenyewe katika mahojiano na kituo kimoja cha runinga nchini Marekani alitolea ufafanuzi suala hilo na kusema kuwa malipo kwa Wanawake hao wawili yalitoka katika fedha zake binafsi na si fedha za kampeni kama inavyodhaniwa na wengi.

Trump amekuwa akimshutumu Cohen kwa kusema mambo yasiyo na ukweli dhidi yake kwa lengo la kupata huruma na kuepuka kifungo.

Kwa mujibu wa sheria za uchaguzi nchini Marekani, malipo yanayofanywa kwa siri kwa niaba ya mwanasiasa ama mgombea yeyote yanaweza kuchukuliwa kama ukiukwaji wa sheria za kampeni za uchaguzi.