Rais wa Algeria arejea kwenye matibabu Ujerumani

0
159

Rais Abdelmadjid Tebboune wa Algeria ameondoka nchini humo kuelekea nchini Ujerumani kwa ajili ya kupatiwa  matibabu, zikiwa zimepita siku chache tangu arejee nchini humo kutoka Ujerumani kupatiwa matibabu.

Kwa muda wa takribani miezi miwili, Rais Tebboune amekuwa akipatiwa matibabu ya corona nchini Ujerumani mpaka tarehe 29  mwezi Desemba mwaka 2020 aliporejea nchini humo.

Habari zaidi kutoka nchini Algeria zinaeleza kuwa, akiwa nchini Ujerumani, Rais Tebboune mwenye umri wa miaka 75 pia atapata matibabu ya miguu ambayo imekuwa ikimsumbua kwa muda mrefu.

Kutoonekana hadharani kwa Rais huyo wa Algeria  kwa takribani miezi miwili, kumezusha hali ya wasiwasi miongoni mwa raia wa nchi hiyo ambao wengi wao hawaamini kama anaweza kumaliza muda wake wa uongozi katika muhula wake wa kwanza.

Rais Tebboune aligundulika kuambukizwa virusi vya corona mwezi Oktoba mwaka 2020.