Mazishi ya pamoja yafanyika Sri Lanka

0
480

Sri Lanka imefanya mazishi ya kwanza ya pamoja ya watu waliokufa katika mfululizo wa mashambulio ya mabomu ya kujitoa muhanga, yaliyotokea kwenye Makanisa na hoteli kadhaa wakati  wa Sikukuu ya Pasaka.

Mazishi hayo ya pamoja ya miili  ya watu Thelathini, yamefanyika katika kanisa la Mtakatifu Sebastian, lililopo kwenye mji wa Negombo, kanisa ambapo nako kulitokea shambulio la bomu la kujitoa muhanga.

Mazishi hayo yamefanyika wakati  Sri Lanka ikifanya maombolezo ya siku moja, kuwakumbuka watu wote waliokufa katika tukio hilo.

Wakati hayo yakiendelea, Polisi nchini Sri Lanka wamesema kuwa idadi ya watu waliokufa katika mashambulio hayo imeongezeka na kufikia 310  na wengine takribani  Mia Tano wamejeruhiwa.

Serikali ya Sri Lanka  inakishutumu kikundi cha Kiislam cha Thowheed Jamath (NTJ) cha nchini humo kwa kuhusika na mashambulio hayo kwa kusaidiwa na vikundi vingine vikubwa vya kigaidi.

Hadi sasa watu 40 wanashikiliwa na Polisi nchini Sri Lanka kwa tuhuma za kuhusika na mashambulio hayo ya mabomu ya kujitoa muhanga kwenye Makanisa na hoteli kadhaa nchini humo.