Kirusi cha ajabu chaibuka nchini China, watatu wafariki

0
556

Mamlaka nchini China zimeripoti visa vipya 139 vya kirusi cha ajabu kilichoibuka siku za karibuni nchini humo na kutia wasiwasi juu ya hali ya afya za wananchi hasa wakati huu nchi hiyo ikielekea kwenye sherehe ya mwaka mpya (Januari 25).

Kwa mara ya kwanza kirusi hicho kimeripotiwa nje ya Mji wa Wahun ambapo ndipo kiligundulika kwa mara ya kwanza Disemba 2019, na sasa kipo katika miji ya Beijing na Shenzhen.

Mbali na China tayari Thailand, Japan na Korea Kusini zimeripoti uwepo wa kirusi hicho kinachofahamika kwa jina la Corona. Tayari watu watatu wamefariki dunia kutokana na matatizo ya mfumo wa upumuaji, huku visa vilivyothibitishwa vikiwa ni zaidi ya 200.

Mamlaka za afya nchini China zimewatoa hofu wananchi na kuahidi kushughulikia tatizo hilo wakati mamilioni ya watu watakapokuwa wakisafiri kutoka maeneo mbalimbali kwenda kuungana na familia zao ili kusherehekea mwaka mpya (Lunar New Year).

Inadaiwa kuwa kirusi hicho kilichozuka mjini Wahun kilianzia kwenye soko la vyakula vya bahari lililopo mjini humo.