Hatua zaanza kuchukuliwa dhidi ya ugonjwa wa Ebola nchini

0
806

Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto imeanza kuchukua hatua za dharura za kukabiliana na ugonjwa wa Ebola katika mikoa iliyo mpakana na Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo    -Drc.

Akizungumza na wananchi Mkoani Katavi, Afisa Programu wa Mawasiliano ya Afya kutoka Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto, Tumaini Haonga amesema mpaka sasa hajaripotiwa mgonjwa yeyote wa Ebola hapa nchini na kwamba tayari wameweka mikakati ya kukabiliana na mlipuko wa ugonjwa huo wakati wowote.

Katika mkutano wa dharura na uhusishaji jamii dhidi ya tishio la mlipuko wa ugonjwa wa Ebola, Idara ya Afya Mkoa wa Katavi kupitia kwa Mganga Mkuu wa mkoa huo Dakta Omary sukali anasema wamejipanga kukabiliana na mlipuko wa ugonjwa huo wa Ebola wakati wowote.

Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto imeanzisha vituo vya kuhudumia wagonjwa wa Ebola Mkoani Katavi kituo pekee ni Kituo cha Karema ufukweni mwa Ziwa Tanganyika.

Serikali pia imefanya maandalizi ya kutosha ya kuwa na wataalam wanaoweza kutoa huduma za dharura kukabiliana na ugonjwa hatari wa Ebola.

Tayari watalaam kutoka Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto wamesambaa katika mikoa ya Katavi, Kigoma, Mwanza, Kagera, Rukwa, Songwe, Mbeya, na Dar es salaam kwa lengo la kuwajengea uwezo wananchi na tishio la ugonjwa wa Ebola hapa nchini.