A-level kusoma hadi miaka mitano

0
469

Wanafunzi nchini Uganda watakaofaulu kujiunga na elimu ya juu ya sekondari [A-Level] wataweza kusoma hadi miaka mitano, ikiwa serikali ya nchi hiyo itaidhinisha mtaala mpya wa elimu kwa A-Level.

Kwa sasa wanafunzi nchini Uganda wanasoma kidato cha tano na sita kwa muda wa miaka miwili kabla ya kujiunga na elimu ya juu ya chuo kikuu.

Kwa mujibu wa mapendekezo ya marekebisho ya mtaala wa A-Level, muda wa kusoma utakuwa usiopungua miaka miwili na usiozidi miaka mitano.

Kwa mwanafunzi ambaye hatafaulu mitihani ya elimu ya juu ya sekondari ya Unganda [UACE] atatakiwa kurudia somo ambalo hajafaulu na sio masomo yote tofauti na hapo awali ambapo ikiwa mwanafunzi alishindwa kupata ufaulu wa masomo mawili alitakiwa kurudia mitihani yote.

Mkurugenzi wa Uhakiki wa Mitaala na Vifaa vya Kufundishia katika kituo cha Kitaifa cha Maendeleo ya Mitaala (NCDC), Berbadette Nambi ameliambia jarida la Saturday Monitor kuwa kipengele hicho cha miaka mitano ni kumwezesha mwanafunzi ambaye hataweza kumaliza A-level katika kipindi cha miaka miwili kurudia mitihani yake ndani ya muda wa miaka mitano ili kupunguza idadi ya wanafunzi wanaoshindwa kuendelea na masomo kutokana na kufeli mitihani hiyo.