Wafanyabiashara wa Tanzania na Ubelgiji kukutana

0
2111

Kongamano la wafanyabiashara wa Tanzania na Ubelgiji linatarajiwa kufanyika jijini Dar es salaam Oktoba 25 hadi 27 mwaka huu na kushirikisha zaidi ya kampuni arobaini na wafanyabiashara wakubwa takribani mia mbili.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es salaam,  Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa  Afrika  Mashariki Dkt Damas Ndumbaro amesema kuwa kongamano hilo lina lengo la kujenga uzoefu na kutangaza fursa za uwekezaji na biashara zilizopo kati ya mataifa hayo.

Amesema kuwa Tanzania na Ubelgiji zimekuwa na ushirikiano mkubwa wa masuala ya uwekezaji, hivyo kufanyika kwa kongamano hilo kunazipa fursa nchi hizo kuimarisha uhusiano wao uliodumu kwa muda mrefu.

“Serikali za Tanzania na  Ubelgiji  zinatekeleza miradi  32 ya biashara na uwekezaji  katika sekta mbalimbali  ambayo ipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji yenye thamani ya dola 902.01 za Kimarekani  ambayo itatengeneza ajira kwa watanzania zaidi ya 1814”, amesema Dkt Ndumbaro.

Akizungumzia sekta ya utalii,  Dkt Ndumbaro amesema kuwa hivi sasa Tanzania na Ubelgiji  wameanza kujadili mikataba mbalimbali ya utalii na endapo itasainiwa itakuwa na manufaa makubwa kwa kuongeza pato la Taifa, ambapo takwimu zinaonyesha kuwepo kwa ongezeko la watalii elfu sita kutoka 7,057 mwaka 2012 hadi kufikia watalii 12,253 mwaka 2017.

Kwa upande wake balozi wa Ubelgiji nchini, Peter Van Acker amesema kuwa kongamano hilo litaipatia fursa nchi yake ya kuimarisha mahusiano ya kidiplomasia na kibiashara na Tanzania, kwa kuwa wafanyabiashara wengi wa nchi hiyo wamekuwa na mwamko mkubwa wa kuzifahamu fursa za uwekezaji zilizopo Tanzania.

“Mkutano huu utaimarisha mahusiano yetu ya kidiplomasia na kibiashara, hivyo tuna mategemeo makubwa kwa wafanyabiashara hawa wakikaa pamoja watabadilishana uzo