Waafanyabiashara soko la Magomeni wapewa siku 7 kuhamia soko jipya

0
278

Manispaa ya Kinondoni mkoani Dar es salaam imetoa muda wa wiki moja kwa Wafanyabiashara wa soko la Magomeni kuhakikisha wanahamia katika soko jipya la Magomeni kama Serikali ilivyokusudia.

Meya wa Manispaa ya Kinondoni Mstahiki Songoro Mnyonge ametoa agizo hilo wakati akitoa ufafanuzi kuhusu matumizi ya soko jipya la Magomeni ambalo limeanza kutumika siku tano zilizopita.

Meya mnyonge amesema, kwa sasa Manispaa ya Kinondoni inakamilisha ujenzi wa sehemu ya kuegesha magari na ujenzi wa mabanda ya kuku, ili kila mfanyabiashara awe na eneo zuri la kufanyia shughuli zake.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Dar es salaam Kate Kamba amesema, kuanza kutumika kwa soko hilo ni utekelezaji wa Ilani ya chama hicho ya kuwajengea maeneo bora ya kufanyia biashara Wananchi wake.

Diwani wa kata ya Mzimuni Manfred Lyoto ambapo ndio soko hilo limejengwa amesema kuwa miradi yote iliyo katika kata hiyo imeanza kutoa matunda, kwa Wananchi kuwa na maeneo bora ya kufanyia biashara.