Kamera za ulinzi elfu 15 kutambua sura Qatar

0
1041

Kamera elfu 15 zenye teknolojia ya utambuzi wa sura zitatumika katika viwanja nane vitakavyotumika wakati wa michuano ya kombe la FIFA la Dunia nchini Qatar itakayoanza tarehe 20 mwezi huu.

Kamera hizo zitakuwa zikiwafuatilia wachezaji na watu mbalimbali watakaoingia ndani ya viwanja hivyo.

Kwa mujibu wa Afisa Mkuu wa Teknolojia wa kombe la FIFA la Dunia 2022, Niyas Abdulrahiman, matukio yote yatafuatiliwa na kurekodiwa na kamera hizo zenye teknolojia ya utambuzi wa sura ambazo zitatumika kutoa taarifa ya mtu kwa kutambua sura yake.

Ufuatiliaji huo unatajwa kuwa sehemu ya juhudi za Qatar za kukabiliana na vitisho vya usalama kama vile ugaidi na uhuni wakati wa mashindano hayo yanayotarajiwa kuhudhuriwa na wageni zaidi ya milioni moja.

Teknolojia hiyo itaendeshwa na Kituo cha Udhibiti na Ufuatiliaji cha ASPIRE ambacho ndicho chenye dhamana ya kusimamia viwanja hivyo nane.

Maeneo mengine yatakayopewa kipaumbele ni vituo vya treni na mabasi.