Mitambo ya Madini yajengwa Dodoma, Mwanza, Geita

0
132

Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Hemed Suleiman Abdulla amesema mitambo mitatu ya usafishaji wa madini ya dhahabu na fedha imejengwa katika Mikoa ya Dodoma, Mwanza na Geita. Ikiwa na uwezo wa kusafisha kilo 965 kwa siku.

Abdulla ameyasema hayo wakati wa ufungaji wa maonesho ya Sita ya Kimataifa ya Teknolojia ya Madini mkoani Geita.

“Mitambo hiyo itawezesha madini ya dhahabu na fedha kusafishwa kwa asilimia 99.99 na kupata thamani halisi ya madini. Jambo hili litawezesha nchi yetu kupitia Benki Kuu kuendelea kununua madini na kuyahifadhi ili kuimarisha shilingi yetu na uchumi wa Tanzania.” – amesema Abdulla.

Abdulla amemwakilisha Rais Samia Suluhu Hassan kwenye ufungaji wa maonesho ya Sita ya Kimataifa ya Teknolojia ya Madini mkoani Geita yaliyoanza Septemba 20, 2023 na kufungwa rasmi leo Septemba 30, 2023.