Mwili wa Christian Atsu wakutwa kwenye kifusi Uturuki

0
439

Christian Atsu, raia wa Ghana aliyekuwa akicheza soka nchini Uturuki amekutwa amefariki dunia siku 12 baada ya tetemeko la ardhi, wakala wake amethibitisha.

“Mwili wa Atsu umekutwa chini ya kifusi,” Murat Uzunmehmet amewaambia waandishi wa habari.

Atsu ambaye alizaliwa mwaka 1992 alitarajia kwenda Ufaransa saa chache kabla ya tetemeko, lakini kocha wake wa Hatayspor amesema alibatilisha uamuzi wake baada ya siku ya Ijumaa kufunga goli la ushindi katika mchezo wa Super League.

Kupitia mitandao ya kijamii watu mbalimbali wameeleza kuguswa na kifo hicho ambacho ni sehemu ya watu zaidi ya watu 45,000 waliofariki kutokana na janga hilo.

Nyota huyo mwenye miaka 31 amewahi kucheza klabu mbalimbali ikiwemo Chelsea, Everton, New Castle United na Bournemouth za nchini England.