TUMEFANYA UTAFITI “chanzo ni malezi”

0
200

Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) Sylvester Mwakitalu amesema kutokana na uwepo wa matukio mengi ya watoto kufanyiwa vitendo vya ukatili na watoto kukinzana na sheria, ofisi yake ilifanya utafiti na kugundua kitu kinachochochea matukio hayo ni malezi.

“Sisi tunaratibu upelelezi lakini tuliamua twende mbali zaidi ili tuone kwa nini mambo haya yanakuwa yanajirudia, tukagundua mengi la kwanza ni malezi ambayo hayafai kama kichochezi kikuu.” amesema DPP

Mkurugenzi huyo wa Mashtaka ameyasema hayo wakati wa mahojiano na TBC1 katika kipindi cha Jambo Tanzania.

Kufuatia kuongezeka kwa matukio hayo, DPP Mwakitalu amewataka Watanzania kuzingatia malezi ya watoto ili kuwalinda na mazingira hatarishi kama ilivyobainishwa katika sheria ya mtoto ya Tanzania kuwa moja ya haki za mtoto ni kulindwa.

“Jamii irudi kwenye kubeba jukumu la kuhakikisha kwamba watoto tunawalea na tunawalinda ili waje kuwa raia wema na wasije kuwa mzigo kwa Taifa.” amesema DPP Mwakitalu

Kwa upande wa watoto nchini, DPP amewakumbusha kutimiza wajibu wao wa kuwa raia wema ndani ya Taifa lao.