Makamu wa Rais amwakilisha Rais Samia Marekani

0
530

Makamu wa Rais, Dkt. Philip Mpango amewasili Jijini New York nchini Marekani ambapo anatarajiwa kumwakilisha Rais Samia Suluhu Hassan katika Mkutano wa Baraza Kuu la 77 la Umoja wa Mataifa (UNGA).

Makamu wa Rais anatarajiwa kuhutubia Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa katika Ukumbi wa Mikutano wa Umoja wa Mataifa Jijini New York nchini Marekani Septemba 22, 2022.

Aidha, ataongoza Ujumbe wa Tanzania katika Mikutano mbalimbali inayohusu Uchumi, Elimu, Afya, Demokrasia na Malengo ya Maendeleo Endelevu ambayo Tanzania imealikwa na nchi washirika, Taasisi za kimataifa na Asasi binafsi.

Katika hatua nyingine Makamu wa Rais amewapongeza Watanzania waishio Marekani kwa jitihada wanazofanya za kuchangia maendeleo katika sekta mbalimbali na kwamba Serikali ya awamu ya sita inatambua mchango wa wana diaspora hao na itaendelea kuunga mkono jitihada wanazofanya.

Aidha, amesema kutokana na lugha ya Kiswahili kuanza kutumika katika Jumuiya mbalimbali kama lugha rasmi, Diaspora wanapaswa kuendeleza lugha hiyo kwa kuitangaza na kuanzisha vituo vya kujifunzia lugha ya Kiswahili katika maeneo waliopo. Makamu wa Rais amesema suala la utangazaji wa lugha ya Kiswahili linapaswa kwenda sambamba na kutangaza utamaduni wa taifa la Tanzania pamoja na vivutio vizuri vilivyopo