Wazee waomba Sensa itumike kuboresha huduma za afya

0
164

Baadhi ya wazee katika kijiji cha Nambunga wilaya ya Newala mkoani Mtwara wameomba baada ya zoezi la sensa ya watu na makazi kukamilika, serikali iboreshe huduma za afya kwa wazee.
 
Wakizungumza kwenye mkutano wa hadhara wa kuhamasisha sensa wamesema upatikanaji wa uhakika wa dawa katika hospitali uzingatie idadi ya wazee kwa kuwa tayari serikali itakuwa imepata takwimu sahihi za wazee kwa kila eneo.
 
Wamesema mara kadhaa wanapofika katika vituo vya kutolea huduma za afya wamekuwa wakikaa kwenye foleni kwa muda mrefu na pia unapofika wakati wa kupata huduma za dawa huambiwa dawa hakuna.
 
Akizungumzia mikakati ya serikali baada ya sensa ya watu na makazi,Waziri  wa Nchi Ofisi ya Rais Kazi Maalum George Mkuchika amesema serikali itaanza kusambaza dawa kulingana na idadi ya watu kila wilaya ili kuondoa changamoto ya uhaba wa dawa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya.