IGP Wambura afanya mabadiliko polisi

0
145

Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini Camillus Wambura,
amefanya mabadiliko madogo kwa baadhi ya makamanda wa polisi ili kujaza
nafasi zilizokuwa wazi.

Nafasi zilizozajazwa zilikuwa wazi baada ya Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama, Rais Samia Suluhu Hassan kuteua na
kuwapandisha vyeo baadhi ya maafisa mwezi Julai mwaka huu.

Waliohamishwa ni Naibu Kamishna wa Polisi Saleh Ambika ambaye
amehamishwa kutoka Kitengo Maalumu cha Upelelezi wa Makosa ya Jinai
kwenda kuwa Naibu Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai kuchukua
nafasi ya Kamishna Faustine Shilogile aliyekuwa akishikilia nafasi hiyo
ambaye aliteuliwa na kupandishwa cheo kuwa Kamishna wa
Kamisheni ya Polisi Jamii.

Kamishna Msaidizi wa Polisi Philemon Makungu amehamishwa
kutoka Mkuu wa Operesheni mkoa wa Kigoma kuwa kamanda wa polisi wa
mkoa huo kuchukua nafasi ya Kamishna wa Polisi Ramadhani Kingai ambaye
alipandishwa cheo kuwa Kamishna wa Polisi na Mkurugenzi wa Upelelezi wa
Makosa ya Jinai.

Kamishna Msaidizi wa Polisi Janeth Magomi amehamishwa kutoka
kamanda wa polisi mkoa wa Songwe kwenda kuwa kamanda wa polisi mkoa
wa Shinyanga, kuchukua nafasi ya Kamishna Msaidizi wa Polisi George
Kyando ambaye amehamishiwa Kamisheni ya Uchunguzi wa Sayansi ya Jinai,
Makao Makuu ya Polisi Dodoma.

Kamishna Msaidizi wa Polisi Alex Mukama ambaye alikuwa Mkuu
wa Upelelezi mkoa wa Shinyanga amehamishwa kwenda kuwa kamanda wa
polisi mkoa wa Songwe.