Serikali na mpango mkakati wa kusimamia Ziwa Victoria

0
226

Serikali imesema itaendelea kushirikia na wataalam wa mazingira kutoka nchini India na maeneo mengine ya dunia kuhakikisha changamoto ya athari za mazingira hususani katika Ziwa Victoria zinapatiwa ufumbuzi wa kudumu kwa manufaa ya nchi.

Hayo yamebainishwa na Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Dkt Selaman Jafo katika hafla ya uzinduzi wa Mpango Mkakati wa Usimamizi Mazingira ya Ziwa Victoria ambapo amebainisha kuwa zaidi watu milioni 40 wanategemea maji ya ziwa hilo hivyo kuhitaji nguvu ya pamoja katika kuulinda.

“Mazingira ya Ziwa Victoria yanakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo ya magugu maji hivyo mpango makakati huu unakwenda kuleta njia sahihi ya kutatua changamoto hizo kwa ajili ya afya ya Watanzania na mataifa mengine yanayotegemea maji ya ziwa hilo,”amesema Jafo.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Baraza la Taifa la Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Dkt. Samuel Gwamaka amesema baraza limeamua kuja na mkakati wa kushirikiana na wataalam wa nje kulinda Ziwa Victoria kutokana na umuhimu wake kwa Taifa na nchi zingine jirani zinazotegemea maji ya ziwa hilo.

Aidha, amewataka wananchi wa ukanda wa ziwa hilo kitumia fursa ya kuwepo kwa wataalam hao nchini kubainisha maeneo mengine yenye changamoto kwenye ili ziweze kutafutiwa ufumbuzi.

Naye Mkurugenzi wa Taasisi ya Sayansi ya mazingira kutoka India, Dkt.Sunita Kumar ameeleza kufurahishwa na hatua mbalimbali zinazochukuliwa na serikali katika kubuni miradi ya maendeleo inayozuia hewa ya ukaa ikiwa ni pamoja na kuzuia matumizi ya mifuko ya plastiki.