Watakiwa kutochagua viongozi kwa ushabiki

0
217

Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Mtwara, Yusuf Nnanila amewataka wanachama wa chama hicho mkoani humo kuacha kuchagua viongozi kwa ushabiki, urafiki au makundi na badala yake wachague viongozi wenye uwezo wa kufanya kazi za chama ili kukiletea maendeleo.

Nnanila ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na waandishi wa habari na kuongeza kuwa chama imara huzaa viongozi na serikali imara ambayo huleta maendeleo kwa wananchi.

Amesema hivi sasa chaguzi mbalimbali ndani ya CCM zinaendelea mkoani Mtwara ikiwemo chaguzi za viongozi kuanzia ngazi za mashina, matawi na kata na kisha ngazi ya wilaya na mkoa, hivyo umakini unahitajika.

Mwenyekiti huyo wa CCM mkoa wa Mtwara ametumia mkutano huo kuwaasa wanachama hao kuacha kufanya kampeni za kuchafuana au kuwachafua viongozi waliopo madarakani, jambo ambalo halileti sura nzuri.