TAKUKURU kuchunguza ujenzi katika zahanati

0
184

Mwenge wa Uhuru umekataa kuweka jiwe la msingi katika ujenzi wa jengo la wagonjwa wa nje (OPD) na maabara katika zahanati ya Marangu wilayani Moshi mkoani Kilimanjaro.

Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru Sahili Nyanzabara ametaja sababu za kutowekwa kwa jiwe la msingi kuwa ni kuchelewa kutekelezwa kwa mradi huo ambapo licha ya fedha kutolewa tangu mwezi wa Oktoba mwaka 2021 lakini mradi umeanza kutekelezwa mwezi Machi mwaka huu.

Kufuatia hali hiyo, Kiongozi huyo wa mbio za Mwenge Nyanzabara amemuagiza Afisa wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Nchini ( TAKUKURU) wilayani Moshi , Casius Kiaro kufanya uchunguzi kuhusu matumizi katika utekelezaji wa mradi huo.

Awali akisoma taarifa ya ujenzi wa mradi huo Mganga mfawidhi wa zahanati ya Marangu, Goodluck Uiso amesema ujenzi huo umegharimu shilingi milioni 250 na utasaidia wananchi kupata huduma za afya kwa karibu.