RUWASA yashusha neema Nanyumbu

0
129

Wakazi wa kijiji cha Namijati wilayani Nanyumbu mkoani Mtwara wamesema ujenzi wa mradi wa maji unaoendelea hivi sasa katika kijiji hicho utafungua ukurasa mpya wa maisha yao, kwani hawajawahi kuona maji ya bomba tangu kupatikana kwa Uhuru.

Wakizungumza na TBC kwa nyakati tofauti, Wakazi hao wamesema kukamilika kwa mradi huo kutachangia katika kuwaongezea kipato, kwa kuwa wamekua wakitumia muda mwingi kwenda kutafuta maji badala ya kushiriki katika shughuli za uzalishaji mali.

Mradi huo unaotekelezwa na Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) kupitia fedha za Mpango wa Maendeleo kwa ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya UVIKO -19, kwa sasa umewasaidia Wakazi hao kupata ajira za muda.

Hadi kukamilika kwake mradi huo utakuwa umegharimu zaidi ya shilingi bilioni moja, huku zaidi ya wakazi elfu tano wakitarajiwa kunufaika na huduma ya maji safi na salama.