Waziri Mchengerwa kukutana na wadau wa sanaa

0
147

Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo Mohamed Mchengerwa amesema anatarajia kukutana na wasanii wa makundi yote katika kipindi kifupi kijacho ili kujua changamoto zinazowakabili kwenye kazi zao ili kupata ufumbuzi wa pamoja.

Mchengerwa ameyasema hayo leo Februari 3, 2022 wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi Mtendaji wa Multichoice Tanzania, Jacqueline Woiso katika ofisi za Wizara Mtumba jijini Dodoma.

Amefafanua kuwa ili kuleta mapinduzi katika sanaa kuna haja ya Serikali kukaa pamoja na wadau ili kujua changamoto na kuzitatua kwa pamoja.

“Nitahakikisha tunakwenda kuwanyanyua na kuboresha kazi za wasanii wetu na kuziweka katika ubora wa kimataifa kwa kushirikiana nao ili wafaidike na kazi zao” amesisitiza Mchengerwa.