Ujenzi daraja la kitengule wafikia asilimia 90

0
244

Serikali imeahidi kuendelea kuboresha miundombinu katika maeneo yenye uwekezaji mahiri yakiwemo yale ya viwanda vyenye kuchochea ukuaji wa uchumi wa nchi.

Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Prof. Makame Mbarawa amesema hayo mara baada ya kukagua ujenzi wa daraja la Kitengule linalouganisha wilaya ya Misenyi na Karagwe ambalo limekamilika kwa asilimia 90.

Daraja hilo linalogharimu kiasi cha shilingi bilioni 25. 5 ni kiunganishi kikubwa cha kusafirishia miwa kutoka mashambani kwenda kiwanda cha sukari cha Kagera na kurahisisha uchumi wa wananchi wa mkoa huo.

Kwa upande wake meneja wa Tanroads mkoa wa Kagera Mhandisi Yudas Msango, amesema tayari mkandarasi amelipwa pesa zote ili kumaliza ujenzi uliobaki wa asilimia 10.

Mwenyekiti wa bodi ya wakurugenzi wa kiwanda cha sukari Kagera, Seif Seif, ameishukuru Serikali kwa kukamilisha ujenzi wa daraja hilo ambalo litarahisisha usafirishaji wa miwa na kuiwezesha kiwanda hicho kuongeza uzalishaji.

Akiwa mkoani Kagera Waziri Mbarawa pia ametembelea kiwanda cha sukari cha Kagera na kujionea uwekezaji uliofanywa zikiwemo huduma za kijamii kama shule ya awali na zahanati.