Diaspora kupewa hadhi maalum

0
108

Serikali iko katika hatua ya uchambuzi wa maoni kwa ajoli ya kukamilisha mchakato wa hadhi maalum kwa Watanzania wanaoishi nje ya nchi (Diaspora)kabla ya kuupeleka bungeni, ili kuwawezesha kushiriki na kuchangia maendeleo ya nchi.
 
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula ametoa kauli hiyo huko Roma, Italia wakati akizungumza na Jumuiya ya Watanzania waishio nchini humo.
 
Amesema tayari mchakato wa awali wa kukusanya maoni kutoka kwa Wadau wote wakiwemo Diaspora umekamilika, na sasa wataalam wako katika hatua za uchambuzi wa maoni hayo.
 
Balozi Mulamula ameongeza kuwa mchakato wa hadhi maalum utakapokamilika utatoa haki za kiraia kwa Watanzania waishio nje ya nchi, isipokuwa kushiriki katika siasa kwa kuwa suala hilo linahitaji mapitio ya kikatiba. 
 
Amewaeleza Watanzania hao wanaoishi nchini Italia kuwa Rais Samia Suluhu Hassan anatambua mchango unaofanywa na Diaspora katika kujitafutia maendeleo yao na kuwataka kuendelea kuwa wazalendo kwa kushiriki katika kuijenga Tanzania kwa kuitangaza vyema kibiashara na kuleta wawekezaji katika sekta mbalimbali.