Dkt. Rioba: Vyombo vya habari viandae vipindi vya kizalendo

0
182

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), Dkt. Ayub Rioba Chacha amewataka waandaji wa vipindi vya elimu kwa umma kuwa wazalendo na kutumia weledi kwa maslahi ya Taifa wakati wakuandaa vipindi.

Akiwasilisha mada kwenye mkutano wa 105 wa washitiri jijini Arusha amesema ni vyema wakatumia takwimu na tafiti zitakazoleta tija kwa nchi.

“Vyombo vyetu vya habari lazima viweze kusimamia ajenda za Taifa letu na tusitegemee ipo siku kuna wengine watakuja kutusaidia kusimamia ajenda zenye maslahi mapana kwa nchi yetu,” ameongeza Dkt. Rioba

Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano kwa Wateja wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa (AICC), Asah Mwambene amesema suala la uzalendo ni muhimu katika kuandaa maudhui.

Washitiri nao wameahidi kutumia ujuzi walioupata kwenye mkutano huo wa siku tano unaoendelea, kuandaa vipindi vyao. Kaulimbiu ya mkutano huo ni Vyombo vya Habari na Mawasiliano kwa Maslahi ya Taifa.