TBC kusikika mipaka ya nchi jirani

TBC-Tanzania

0
315

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Innocent Bashungwa na Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Dkt. Faustine Ndugulile wamezindua kituo cha kurushia matangazo ya TBC Taifa na TBC FM kilichopo tarafa ya Kisaki Kijiji cha Sesenga wilayani Morogoro.

Kuzinduliwa kwa kituo hicho ambacho ujenzi wake umegharimu kiasi cha shilingi milioni 450 kitawanufaisha wananchi wa vijiji vya wilaya hiyo pamoja na eneo la ujenzi wa mradi wa bwawa la kufua umeme la Julius Nyerere kupata usikivu wa matangazo ya moja kwa moja kutoka Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC)

Baadhi ya vijiji wilayani Morogoro vimekosa huduma ya usikivu wa matangazo kutoka TBC kwa muda mrefu, sasa serikali kupitia wizara mbili za kisekta na taasisi zake ikiwemo Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) na TBC imelazimika kufikisha huduma hiyo katika wilaya hiyo.

Katika uzinduzi na makabidhiano ya kituo cha kurusha matangazo Waziri Bashungwa na Waziri Ndugulile wameeleza malengo ya serikali katika kufikisha huduma hiyo ambayo ni kuhakikisha kila wilaya zinafikiwa na matangazo ya moja kwa moja ya Shirika la Utangazaji Tanzania zikiwemo wilaya zilizopo mipakani mwa nchi jirani.