Rais azindua hospitali ya kijeshi Dar es Salaam

0
156

Rais Samia Suluhu Hassan leo Julai 28, amezindua Hospitali ya Kijeshi ya Magonjwa ya Kuambukiza na Mlipuko iliyopo Lugalo mkoani Dar es Salaam ikiwa ni hospitali ya namna yake katika kukabiliana na magonjwa hayo.

Hospitali hiyo ambayo si tu kwa ajili ya wananjeshi bali pia itawatibu wananchi wote na pia itatumika kama kituo cha kufanyia tafiti za kisayansi pamoja na mafunzo kwa ajili ya wanafunzi wa masomo ya sayansi.

Rais Samia Suluhu Hassan ameelezwa kuwa hospitali hiyo ni ya kipekee kwani imejitenga na makazi ya wananchi, imezungukwa na uzio kote na kuwa na mifumo ya kiusalama hivyo inafaa zaidi katika kukabiliana na magonjwa ya mlipuko na pia mgonjwa hatoweza kutoka au mtu mwingine kuingia kwa urahisi.

Ujenzi wa hospitali hiyo umechukua miezi nane na umegharimu shilingi bilioni 10.5, ikiwa ni ufadhili kutoka Taasisi ya Jeshi la Ujerumani (German Army Foundation).

Hospitali hiyo ina uwezo wa kulaza wagonjwa 128 katika mazingira ya kawaida, lakini kunapotolea mlipuko wa magonjwa inaweza kulaza wagonjwa zaidi ya 400, kwa kitumia pia mahema ya kisasa yaliyojengwa.

Hospitali hiyo itashirikiana na hospitali nyingine nchini katika kukabiliana na magonjwa ya mlipuko ili kuhakilisha wananchi wanakuwa salama na wenye afya njema.