Rais Samia ahudhuria mechi ya Simba na Yanga

0
232

Rais Samia Suluhu Hassan leo Julai 3, 2021, amewashtukiza mashabiki wa soka nchini pale alipohudhuria mechi ya watani wa jadi Simba na Yanga.

Rais Samia aliyepokewa uwanjani hapo pamoja na viongozi wengine na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Hassan Abbasi na Rais wa TFF, Wallace Karia, aliingia uwanjani hapo muda mfupi tu kabla ya mechi kuanza na kupokewa na mashabiki wa pande zote mbili kwa miluzi na makofi ya furaha.

Rais Samia alikaa hadi dakika 90 za mchezo zilipomalizika akionesha kwa kiwango kikubwa anavyounga mkono masuala ya michezo na burudani.

Itakumbukwa kuwa wiki iliyopita tu Rais Samia alipiga simu kwenye tamasha la msanii Nandy (Nandy Festival) na kuwatakia wadau wa sanaa na burudani kila la kheri katika tamasha hilo.

Katika mchezo huo Yanga imeibuka mshindi kwa kuifunga timu ya Simba goli moja kwa nunge.

Goli hilo limefungwa na Zawadi Mauya katika dakika ya kumi na mbili kipindi cha kwanza cha mchezo huo.