Watuhumiwa 7 wa dawa za kulevya wafikishwa mahakamani

0
366

Watu saba, raia wa Iran wamefikishwa katika Mahakama ya hakimu mkazi mkoani Lindi kwa tuhuma za kusafirisha dawa za kulevya kinyume cha sheria ya Kudhibiti na Usimamizi wa dawa za kulevya ya mwaka 1995.

Akiwasomea mashtaka watuhumiwa hao, Mwendesha mashtaka Juma Maige ameiambia mahakama kuwa, watu hao wanatuhumiwa kusafirisha dawa za kulevya aina ya Heroin kilo 504.36 na kosa jingine ni kusafirisha dawa za kulevya aina ya Methamphetamine kilo 355.

Watuhumiwa hao ni Jan Mohamen Miran, ssa Baluchi Ahmad, Amir Hussein Kasom Salim Baluchi Fedhmuhammad, Ikbar Pakir Mohamed Mustaphar Nowan Kadir Barksh na Jawid Nuhan Nur mohammad, ambao walikutwa wakisafirisha dawa za kulevya katika bahari ya hindi eneo la Kilwa mkoani Lindi.

Hakimu mkazi mfawidhi wa mahakama hiyo Maria Batulaine amewataka watuhumiwa hao kutojibu chochote, kwa kuwa mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza shauri lao.

Akitafsiri kutoka Kiswahili kwenda lugha ya Kifarsi au Kipersia inayozungumzwa na watuhumiwa hao, Mkalimani Flora Washokera amewaeleza kuwa kwa mujibu wa sheria, makosa wanayotuhumiwa hayana dhamana, na kwamba shauri lao limeahirishwa hadi Mei 14 mwaka huu.