Majaliwa: Watanzania endeleeni kuiamini serikali

0
200

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amewataka Watanzania wendelee kushikamana katika kipindi hiki ambacho dunia ina mahangaiko makubwa na magonjwa mbalimbali ya maambukizi.

”Tuendelee kumtegemea Mwenyezi Mungu kama Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli alivyotusisistiza na tuendelee kuiamini Serikali na jitihada za viongozi wake tutapata utulivu.

Waziri Mkuu ameyasema hayo leo wakati aliposhiriki mazishi ya mfanyabiashara maarufu katika mikoa ya Lindi na Mtwara Ally Nalaga yaliyofanyika Mnazimmoja, Lindi.

Amesema magonjwa hayo yameleta tafsiri tofaiti na wakati mwingine kutokuwa na utulivu kwani watu wanatishana sana na hali ambayo inawafanya wasiwe na amani na kuwajengea hofu.

Waziri Mkuu amesema Serikali inaendelea kufuatilia mwenendo wa aina zote za magonjwa ambayo yanawakabili wananchi katika maeneo mbalimbali nchini na kuyatafutia tiba.

Hata hivyo, amewasisitiza wananchi waendelee kuchukua tahadhari ya kila ugonjwa. ”Ukisikia UKIMWI kuna tahadhari zake, ukisikia kipindupindi kina tahadhari zake.”