Umeme wapunguza matumizi ya mafuta ya taa nchini

0
208

Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani amesema usambazwaji na upatikanaji wa umeme vijijini umepunguza kwa kiasi kikubwa matumizi ya mafuta ya taa nchini.

“Kwa sasa matumizi ya mafuta ya taa yamepungua hadi kufikia takribani lita 110,000 kwa siku tofauti na ilivyokuwa huko nyuma, ambapo lita zaidi ya 140,000 zilikuwa zikitumika kwa siku na hii inatokana na shughuli nyingi za kijamii vijijini kutumia umeme,” Amesema Dkt. Kalemani

Ameongeza kuwa, mafuta ya taa yalikuwa yakitumika kama chanzo cha mwanga vijijini, ambapo sasa asilimia kubwa ya wakazi wa vijijini wanatumia umeme kujipatia mwanga.

Kuhusu kuongezeka kwa matumizi ya mafuta ndege, Dkt. Kalemani amesema kuwa kwa sasa matumizi ya mafuta hayo yameongezeka kutokana na kuwepo kwa safari nyingi za ndege zinazomilikiwa na serikali.

“Kwa sasa Tanzania inamiliki ndege nyingi ambazo hufanya safari zake ndani na nje ya nchi, hivyo kufanya mafuta hayo kutumika kwa wingi.”

Amefafanua kuwa, matumizi ya mafuta ya ndege yamepanda hadi kufikia lita laki 6 ambapo huko nyuma matumizi yalikuwa chini ya lita laki 3 kwa siku.

Katika hatua nyingine, amesema kuwa, Serikali inaendelea na mpango wa kuanzisha vituo vidogo vya mafuta katika maeneo ya vijijini ili kusogeza karibu huduma ya mafuta ya petroli, dizeli na taa.